Skip to main content

KUFUNGWA KWA SOKO YA BURMA NI FURAHA WAKAAZI WA NAIROBI

Mtunzi: Odhiambo Danyell

Ni bayana kwamba wenyeji wa Nairobi na vitongoji vyake wana kila
sababu ya kutabasamu baada ya tangazo la kufungwa kwa soko maarufu la
nyama kwa jina Burma. Hatua hii imechochewa na  tabia ya  wafanyi
biashara kukaidi kutii sheria za wakaguzi wa afya.

Kabla ya kungamua hatari inayowakodolea macho walamba minofu katika
soko hilo ni heri nikufafanulie taswira halisi angalau ufahamu
chimbuko la  hatua hii. Punde tuu unapofika katika lango kuu la soko
hilo utakaribishwa na harufu mbaya inayoninginia hewani.

Kando na hayo, utashuhudia jaa kubwa la taka la kusheheni pembe za
wanyama, makombo ya minofu pamoja na maji taka iliyozagaa kila sehemu.
Hatimaye, utawaona chokora wakibishana na mbwa ambao hukukwangura jaa
hilo wakitafuta pato lao.

Kuingia ndani, utapishana na wafanyi biashara wa nyama waliovalia
ovaroli chafu za kutona damu wakibeba bidhaa hiyo kiholela huku
wakivuka mitaro iliyosakamwa na maji taka iliyoganda wakati
wakisindikizwa na vikosi vya nzi.

Aidha, kwenye maduka na hoteli , hutakosa kujionea jeshi kubwa  la nzi
ambao  wameteka nyara kila sehemu hata kuwalazimisha wenyeji kurusha
rusha mikono wakati wakiendelea kufurahia mapishi rojorojo ambayo
huandaliwa kwenye hoteli hizo za Burma.

Tushamhoji mgonjwa na sasa hatuna budi kugeukia daktari angaa tupate
tiba kwa hali hii mbaya kwa vile ni wazi, tusipojenga ufa  tutajenga
ukuta. Hivyo, wakati tukiwakemea wafanyibiahsra wa Burma na kukumbatia
hatua ya kufunga soko hilo ni muhimu mikakati kabambe iwekwe ili
kuepusha wenyeji wa soko hilo na mikurupuko ya magonjwa.

Hayo ni tisa, kumi ni kwamba ili kupata suluhisho la kudumu soko hilo
lafaa kubomolewa na hatimaye kujengwa upya huku wakizingatia miundo
msingi za kuimarisha usafi. Aidha, sheria za baraza la jiji pamoja na
zile za wizara husika zinapaswa kukazwa. Mwisho, wenyeji wanapaswa
kufanyiwa hamasisho kuhusu umuhimu wa kudumisha usafi na hatari ya
kuendelea kufanya kazi zao katika mazingira hayo.

Comments

Popular posts from this blog

MAZINGAOMBWE YA SAA

Na Danyell Odhiambo Nimejirusha kwenye kiti kilegevu cha msonobari nikifikiria jinsi hali ya maisha nchini Kenya inavyozidi kupaa kila uchao. Mbele yangu, pametulia redio, kando pamesimama kikombe cha kahawa chungu na juu pananinginia saa ya ukuta. Ghafla, fikra zangu zinatekwa nyara na saa iliyozubaa ukutani. Nikiangazaangaza, naona imetimia usiku mkuu. Hii ni kumaanisha, mishale yote ya saa imekutana kifuani pa namba kumi na mbili. Ukipiga hesabu kwa makini, utakubalina nami kwamba tukio kama hili hujirudia mara mia tatu sitini na tano kila mwaka. Ukumbuke, kisa hiki pia huashiria kuzaliwa kwa siku mpya. Hata ingawa mishale hizi zimedhibitisha ushirikiano ni kiungo muhimu katika katika kikundi, taswira fulani inaibuka nikiangalia mishale hizo. Taswira yenyewe yahusu tabia mbovu ya wabunge kukaidi shinikizo za kuwataka kulipa malimbikizi yao ya kodi. Nikipamabanua kitendawili hiki, itakubali kwamba jamii imejigawanya kupitia mishale hizi tatu za saa. Mahuluku taabu nawafa...

MAPENZI KIZUNGU ZUNGU

MTUNZI: ODHIAMBO DANYELL Mawimbi makali baharini yalikimbizana na hatimaye kusukuma maji hadi ufukweni. Pembeni, Bahati alionekana ameshika kijiti kirefu mkononi akijaribu kuchora umbo la moyo wa mapenzi kwenye changarawe mbichi huku maji ya bahari yakifuta. Angani, ndege aina ya korongo na mbayu wayu wangeonekana wakicheza cheza huku tufani kali zikifanya matawi ya minazi ufuoni kupukutika. Nikijistiri juu ya roshani(balcony) katika hoteli ambayo tulikuwa tumekodisha nilisalia kula kwa macho. Nilibakia kinywa wazi kuona madhari ya kutamanisha jinsi jua ilizama upeoni na kufanya maji ya bahari kupiga rangi ya manjano. mawazoni, nilitawaliwa na picha za harusi yetu jana yake katika ukumbi wa pataneni . Hatua chache niliona suti yangu ambayo ilikuwa ingali sakafuni baada ya usiku yenye sarakasi si kidogo. Ajabu, marashi yenye uhai aliyopiga Bahati ilikuwa bado imesakama pua yangu.Waliosema harusi ni kilele cha mapenzi hawakukosea hata kidogo. “Honey…………Rashidy! Rashidy!” Kwa...

SIRI ZA “JAM” JIJINI NAIROBI; TOLEO LA PILI

MTUNZI: ODHIAMBO DANYELL Jinsi basi lilivyozidi kufukuzia kuelekea mzunguko wa Nyayo stadium, ndivyo ilizidi kuwachilia moshi ya mpingo iliyosokota angani kabla ya kutawanyika. Pale pia, tulimpata polisi wa trafiki mwanamke aliyefungia mshipi wa longi yake kwenye kifua. Amini usiamini, kwa ishara ya mkono alielekeza mkondo wa gari kama jinsi upepo huele ... keza bendera. Pale tulis...imama kwa dakika chache kabla ya msongamano kufunguliwa. Cha kuvutia tamaa ya macho yangu ilikuwa ‘tuk tuk’ fulani ambayo ilipenya penya kati kati ya magari huku ikipiga kelele kama mashine ya kusaga mahindi. Wenzangu wanaiita kule bara POSHOMILL. “We! Boss, ondoa hiyo kabati kwenye barabara” alisikika akishambuliwa na mmoja wa madereva wa matatu. Wanasema muungwana hununa moyoni na wala siyo mashavuni na kwa hivyo Yule dereva wa ‘tuk tuk’ akaridhia kumjibu kwa kimya. Kando na tukio hili, kuna jambo lililotendeka ambalo liliwacha mbavu za kila mtu zikiuma. Niseme nisiseme! Aaaah! ...