Skip to main content

OPERATION TUTETEE WANAUME!!!

MTUNZI: ODHIAMBO DANYELL
SEHEMU YA KWANZA:

Mzee Matendechere alionekana kuokotwa na usingizi mwepesi wakati akiuguza majeraha ya panga hospitalini. Kisa na maana, adabu ilimhama mkewe hata akaamua kuchukua sheria mkononi na kumpa mumewe kichapo cha mbwa kabla ya kutorokea kusichojulikana.

Kichwa chake kilibanwa kwa kilemba cheupe chenye matone ya damu. Isitoshe, Kwenye shavu la kushoto, palidhihirika jeraha bichi lenye kushonwa kwa uzi. Cha kusikitisha zaidi, Pembezoni mwa kitanda, wangeonekana wapiga picha kutoka vyumba vya habari waking’ang’ana kuchukua picha za kuvutia watazamaji.
picha kwa hisani ya http://medievalminds.com


Maskini Matendechere alizidiwa na usingizi hata akabakia kukoroma huku akifungua mdomo mithili ya mamba mwenye njaa. “Wow! This seems to be the best shot, I,m loving this” alisikika akisema mmoja wa wapigaji picha tuliyeshuku ni wa asili ya kimarekani. Kweli, vita vya panzi furaha ya kunguru.

Wakati haya yakijiri, ndoto ya matukio yaliyotendeka kabla ya masaibu haya kumpata Matendechere yalivamia mawazo yake. Akilini, alijaribu kukusanya picha hizo bila ya kitendawili cha asili ya maumivu yake kuteguka.

Midundo mizito ya rumba ilizidi kufagilia katika mkahawa maarufu wa ‘tamasha’ katika barabara ya tugawe umaskini. Kama kuchokoza wenye kuneng’ua viuno kwenye sakafu, Deejay Manyoya aliwachilia kibao maarufu ‘I,m not sober’ cha bendi maarufu ya Jamnazi Afrika. Kauli hii ilisindikizwa na vifijo na nderemo. ungedhani ni karamu ya kukaribisha kurudi kwa Yesu. Haya yakijiri, baadhi ya wenyeji walizidi kumimina chupa za mvinyo macho wakibandika kwenye runinga.

Wakati huu wote, Mzee Matendechere alikuwa amechokorwa kichwa na mizimwi ya mvinyo kiasi ya kwamba aliridhia kutafuta starehe kwenye kochi kando ya ‘counter’.

Ukitizama kushoto, ungeona kundi la makahaba ambao walikuwa wamejikwatua kwatu kwatu wakianika mitego yao tayari kunasa wateja. Mwingine alivalia ‘tumbo cut’ ya kubana kifua yenye maandishi “usiseme maziwa, sema ngombe”. Isitoshe, alivalia sketi fupi iliyofichua mapaja yake yenye madoadoa utadhani ni wa jamii ya chui au fisi.

Wakati viumbe hawa wakisasambua mapaja yao kwa wapita njia, Mzee Matendechere alibakia kuvuta mabaki ya sigara yaliyoangushwa na wateja sakafuni. Baba mtu alizubaishwa na vimulimuli vya taa ya ‘disco light’ akakaribisha moshi ndani ya mapafu kabla ya kuwachilia wingu kubwa hewani.

“Mzee! Inuka uende nyumbani. Tuko karibu kufunga na hatutaki ukamatwe na polisi” wahudumu pale kwenye mkahawa walimrai. “Kwani huyo Mututho anadhani ni nani atupimie starehe na pesa tunakunywa ni zetu? Leta kingfisher mbili hapo.” alisikika Matendechere akizusha kwa ujeuri huku akilaani mbunge aliyebuni sheria inayopima masaa ya kunywa pombe.

Wakati Matendechere akizizana na wale wahudumu , ghafla fikra zake zilivutiwa na maandishi FulanI ukutani. “Customers have a right to stay and to pay”. “Haya ndiyo madhara ya kususia masomo mapema. Can you please read the bold writings on the wall?” Mzee Matendechere aliwakabili huku akionekana kuzidiwa na kichefuchefu.

Kwa dakika zile chache, baba mtu alijiona jogoo wa kukomaa. kuwika kwake kuliwatisha wahudumu. Kwenye lango kuu la mkahawa, tayari wateja wengine wangeonekana wakiondoka wameshikana taratibu kumaanisha walikuwa wameona dalili ya . Kadri masaa yalivyoyoma ndivyo shughuli zilipungua pale hata mziki ikazimwa na stima kuzimwa.

“Ala! Mzee, hii ni siku ya pili tunakutoa hapa kwa nguvu. Kwani huna familia? Enda nyumbani tunafunga.” Askari aliyeshika doria langoni alimzomea Matendechere.

Baadaye, baba mtu aliona amezidiwa maarifa hata akajikusanya na kutembea taratibu akieleka nyumbani. Barabarani, hungempita bila ya kumtambua kutokana na kuimba kwake. “I,m not sober Odiero, I,m not sober……..i,m not sober because I,ve taken guiness.”hivyo ndivyo hali ilikuwa.

Ilibakia kona moja tuu kabla ya kuwasili kwenye maskani yake katika kambi ya wakimbizi wa ndani kwa ndani pale Soweto. Pale, aliteleza na kuanguka kwenye mtaro ya maji taka. “Auuuwi!.... Auuuwi! Mama Wanjiru bwana yako ameingia kwenye mtaro. Njoo tumsaidie” mama mmoja msamaria mwema alipaza sauti na kuvutia umati.

SHUKRAN!!!!
Endelea kufuatilia hadithi hii kujua kinachojiri!!!!!........

Comments

Popular posts from this blog

MAZINGAOMBWE YA SAA

Na Danyell Odhiambo Nimejirusha kwenye kiti kilegevu cha msonobari nikifikiria jinsi hali ya maisha nchini Kenya inavyozidi kupaa kila uchao. Mbele yangu, pametulia redio, kando pamesimama kikombe cha kahawa chungu na juu pananinginia saa ya ukuta. Ghafla, fikra zangu zinatekwa nyara na saa iliyozubaa ukutani. Nikiangazaangaza, naona imetimia usiku mkuu. Hii ni kumaanisha, mishale yote ya saa imekutana kifuani pa namba kumi na mbili. Ukipiga hesabu kwa makini, utakubalina nami kwamba tukio kama hili hujirudia mara mia tatu sitini na tano kila mwaka. Ukumbuke, kisa hiki pia huashiria kuzaliwa kwa siku mpya. Hata ingawa mishale hizi zimedhibitisha ushirikiano ni kiungo muhimu katika katika kikundi, taswira fulani inaibuka nikiangalia mishale hizo. Taswira yenyewe yahusu tabia mbovu ya wabunge kukaidi shinikizo za kuwataka kulipa malimbikizi yao ya kodi. Nikipamabanua kitendawili hiki, itakubali kwamba jamii imejigawanya kupitia mishale hizi tatu za saa. Mahuluku taabu nawafa...

MAPENZI KIZUNGU ZUNGU

MTUNZI: ODHIAMBO DANYELL Mawimbi makali baharini yalikimbizana na hatimaye kusukuma maji hadi ufukweni. Pembeni, Bahati alionekana ameshika kijiti kirefu mkononi akijaribu kuchora umbo la moyo wa mapenzi kwenye changarawe mbichi huku maji ya bahari yakifuta. Angani, ndege aina ya korongo na mbayu wayu wangeonekana wakicheza cheza huku tufani kali zikifanya matawi ya minazi ufuoni kupukutika. Nikijistiri juu ya roshani(balcony) katika hoteli ambayo tulikuwa tumekodisha nilisalia kula kwa macho. Nilibakia kinywa wazi kuona madhari ya kutamanisha jinsi jua ilizama upeoni na kufanya maji ya bahari kupiga rangi ya manjano. mawazoni, nilitawaliwa na picha za harusi yetu jana yake katika ukumbi wa pataneni . Hatua chache niliona suti yangu ambayo ilikuwa ingali sakafuni baada ya usiku yenye sarakasi si kidogo. Ajabu, marashi yenye uhai aliyopiga Bahati ilikuwa bado imesakama pua yangu.Waliosema harusi ni kilele cha mapenzi hawakukosea hata kidogo. “Honey…………Rashidy! Rashidy!” Kwa...

SIRI ZA “JAM” JIJINI NAIROBI; TOLEO LA PILI

MTUNZI: ODHIAMBO DANYELL Jinsi basi lilivyozidi kufukuzia kuelekea mzunguko wa Nyayo stadium, ndivyo ilizidi kuwachilia moshi ya mpingo iliyosokota angani kabla ya kutawanyika. Pale pia, tulimpata polisi wa trafiki mwanamke aliyefungia mshipi wa longi yake kwenye kifua. Amini usiamini, kwa ishara ya mkono alielekeza mkondo wa gari kama jinsi upepo huele ... keza bendera. Pale tulis...imama kwa dakika chache kabla ya msongamano kufunguliwa. Cha kuvutia tamaa ya macho yangu ilikuwa ‘tuk tuk’ fulani ambayo ilipenya penya kati kati ya magari huku ikipiga kelele kama mashine ya kusaga mahindi. Wenzangu wanaiita kule bara POSHOMILL. “We! Boss, ondoa hiyo kabati kwenye barabara” alisikika akishambuliwa na mmoja wa madereva wa matatu. Wanasema muungwana hununa moyoni na wala siyo mashavuni na kwa hivyo Yule dereva wa ‘tuk tuk’ akaridhia kumjibu kwa kimya. Kando na tukio hili, kuna jambo lililotendeka ambalo liliwacha mbavu za kila mtu zikiuma. Niseme nisiseme! Aaaah! ...