Skip to main content

SIRI ZA 'JAM' JIJINI NAIROBI

MTUNZI:ODHIAMBO DANYELL

Dereva wa basi la kampuni ya RWAKEN alijistiri mbele ya usukani na kupiga gari moto wakati tukiondoka katika kitivo cha chuo kikuu cha Daystar yenye makao katika mzunguko wa barabara ya Valley road, Nairobi.

Ilikuwa dakika chache baada ya saa kumi na nusu jioni. Hii ni kumaanisha, wafanyikazi pamoja na wanafunzi wa mchana chuoni tayari walikuwa katika harakati zakufunganya virago na kurejea makwao baada ya panda shuka za mchana.


Vvrrrrrrrrrrrrrm! vvrrrrrrrm! Dereva alipasha gari moto na taratibu basi likaelekezwa nje ya lango kuu. kabla ya kuingia kwenye barabara kuu ya Valley road.

Auuuuuwi! imagine mbele yetu palisimama gari aina ya Range Rover Vogue iliyowachilia moshi nyeupe iliyosokota na kupata hifadhi katika mapua ya basi la RWAKEN. Katika mbuga la wanyama, gari hili linalinganishwa na mfalme Simba kutokana na udhabiti wake. Mashini hii yasifika kwa ulafi wa petroli pamoja na muundo wake wa kutamanisha. Aha! Sasa nimejua kwanini basi ilikuwa inanguruma kama yenye mafua....

Kando na hayo, sisemi nilivutiwa zaidi na rangi yake nyekundu ya kukoza pamoja na ‘rims’ za shaba ukipenda silver na isitoshe magurudumu inchi sita. Kutamanisha zaidi, ilikuwa nambari yake ya usajili KBR 001Z. “Bonge la wallpaper” alisikika mmoja akishangaa ndani ya basi.

Kushoto, palinguruma gari nyingine aina ya Hummer, almaarufu ‘nyundo’. huyu pia ni Ibilisi mwingine katika orodha ya maadui wa petroli. Nikimwita kifaru wa jiji hutanipinga. Maumbile yake, pamoja nasifa yake ya  kutembea kifua mbele inalingana na ubingwa wake.

Mbele alirembeshwa kwa vyuma vya kumetameta. Nyuma alikosa nambari ya usajili hata tukashuku bado mgeni nchini. Kitendawili kumhusu ni uhusiano wake kimapenzi na wanasiasa nchini Kenya.ukitaka umaarufu huna budi kumchombeza.

Kwenye msafara, alifanya magari mengine ya kibinafsi kuonekana kama siafu. sitataja kina kaka Vitz, Alex,Runx, March, Probox orodha ni ndefu taja zingine........

Tuwache hayo. kuna huyu dereva wa vitz aliyeonekana kuwa na haraka na hata akapenyeza kijigari lake kwenye njia ya mguu kando kando hata kuwaudhi wapita njia. utanikashifu kwa kuwa mmbea lakini heri nimfichue.

Hayawi hayawi, hatimaye huwa. Polisi wa trafiki mwenye kitumbo cha kiriba alifungulia magari na taratibu msafara wa magari ulisonga kama jinsi mkondo wa mto huteremka mlima. Ghafla, mkondo ulishika kasi na magari yakapepea kwenye barabara kuu ya mbagathi.

Tulipofikia makutano ya barabara ya Langata, tulipata pamefanyika ajali mbaya sana. Kulingana na mashahidi wa karibu, dereva wa gari hilo aina ya Toyota Caldina alisemekana kupoteza mwelekeo kabla ya kurukia gomba la ndizi kando ya barabara. Gari ilijikunja sura ungedhani imepiga busu domo la gari moshi. "Wololo! Maskini!" alishangaa dereva wa basi.


Comments

Popular posts from this blog

MAZINGAOMBWE YA SAA

Na Danyell Odhiambo Nimejirusha kwenye kiti kilegevu cha msonobari nikifikiria jinsi hali ya maisha nchini Kenya inavyozidi kupaa kila uchao. Mbele yangu, pametulia redio, kando pamesimama kikombe cha kahawa chungu na juu pananinginia saa ya ukuta. Ghafla, fikra zangu zinatekwa nyara na saa iliyozubaa ukutani. Nikiangazaangaza, naona imetimia usiku mkuu. Hii ni kumaanisha, mishale yote ya saa imekutana kifuani pa namba kumi na mbili. Ukipiga hesabu kwa makini, utakubalina nami kwamba tukio kama hili hujirudia mara mia tatu sitini na tano kila mwaka. Ukumbuke, kisa hiki pia huashiria kuzaliwa kwa siku mpya. Hata ingawa mishale hizi zimedhibitisha ushirikiano ni kiungo muhimu katika katika kikundi, taswira fulani inaibuka nikiangalia mishale hizo. Taswira yenyewe yahusu tabia mbovu ya wabunge kukaidi shinikizo za kuwataka kulipa malimbikizi yao ya kodi. Nikipamabanua kitendawili hiki, itakubali kwamba jamii imejigawanya kupitia mishale hizi tatu za saa. Mahuluku taabu nawafa...

OPERATION TUTETEE WANAUME!!!

MTUNZI: ODHIAMBO DANYELL SEHEMU YA KWANZA: Mzee Matendechere alionekana kuokotwa na usingizi mwepesi wakati akiuguza majeraha ya panga hospitalini. Kisa na maana, adabu ilimhama mkewe hata akaamua kuchukua sheria mkononi na kumpa mumewe kichapo cha mbwa kabla ya kutorokea kusichojulikana. Kichwa chake kilibanwa kwa kilemba cheupe chenye matone ya dam u. Isitoshe, Kwenye shavu la kushoto, palidhihirika jeraha bichi lenye kushonwa kwa uzi. Cha kusikitisha zaidi, Pembezoni mwa kitanda, wangeonekana wapiga picha kutoka vyumba vya habari waking’ang’ana kuchukua picha za kuvutia watazamaji. picha kwa hisani ya http://medievalminds.com Maskini Matendechere alizidiwa na usingizi hata akabakia kukoroma huku akifungua mdomo mithili ya mamba mwenye njaa. “Wow! This seems to be the best shot, I,m loving this” alisikika akisema mmoja wa wapigaji picha tuliyeshuku ni wa asili ya kimarekani. Kweli, vita vya panzi furaha ya kunguru. Wakati haya yakijiri, ndoto ya m...

KUMBU KUMBU ZA MWANA HAWA

MTUNZI: Odhiambo Danyell Manyunyu mepesi ya mvua yangesikika yakikung’uta mabati na kuibua mdundo flani iliozidisha tamaa yangu ya  kuendelea kupanga mbavu kwenye kitanda. Mara, alisikika jogoo mmoja kijijini akiwika kama kuashiria nuru ilikuwa imekubali zamu yake ya mchana. Nilibaki kugaragara kitandani huku mabishano makali yakiendelea akilini kati ya mwili dhaifu na nafsi yangu. Mwili ilisisitiza niendelee kulala huku nafsi ikinisihi niamke. Baada ya kutafakari kuhusu hasara za usingizi niliridhia kuamka. Ghafla, fikra zangu zilielekezwa katika saa kubwa iliyoning'inia ukutani ambayo ilikatiza hali ya unyamafu uliokuwa umetawala chumbani. kuzidisha, chenene fulani aliyekuwa kajificha mvunguni alianza kutoa sauti ya kuudhi. “Aah! Heri tuu niamke” nilijisemeza huku nikijikokota kuelekea kwenye dirisha. Nikichungulia nje, ningeona kunguru wakipigania makombo ya chakula kwenye pipa iliyosimama mkabala na chumba changu. Isitoshe, rukwama kukuu za wazegaz...