Skip to main content

MAKARIBISHO YA WANAFUNZI WAGENI CHUONI DAYSTAR!

Hayawi! Hayawi! Hatimaye huwa. Msafara mrefu wa magari ya kifahari ulitawala barabara kuu ya mchanga kuelekea katika lango kuu la chuo cha Daystar, Athiriver. Kwangu ilikuwa ni kama jonzi kwani maishani halikuwahi kunidara wazo kwamba siku ingenijia ya kujiunga na chuo hili maaarufu.

Nikijisitiri kwenye piki piki moja kuu kuu ambayo ilinikumbusha kisa cha punda mzee aliye rusha mateke, kupiga nduru na kulia machozi alipofanyishwa kazi ya sulubu bila ya mwenyewe kujali.vivyo hivyo pikipiki ilisikika kuyumba yumba huku ikitoa sauti kubwa na moshi ya mpingo iliyosokota angani bila ya dereva kushtuka.



Wakati mbwe mbwe na shamra shamra zikitawala tulipofikia msafara huo katika lango kuu chuoni humo sikuwachwa nyuma kwani niliwasili kwa ‘style’ya aina yake. Godoro niliifunga mgongoni, begi kubwa yenye picha kubwa ya "rambo" ikiniwekelea tako utosini na ndoo ikininginia taratibu begani. Zaidi, dereva wa pikipiki alitia nakshi taswira hii kwa kuwasili kwa kishindo kikubwa.

Alipiga honi na breki ya ghafla iliyotifua wingu la vumbi kama kuashiria “hata sisi tumecome”
“Habari zenu?” askari mmoja aliyeshika doria langoni aliuliza kwa sauti dhabiti.
“Za kwetu salama, labda utujuze za kwako?” dereva wa piki piki alidakia kwa unyenyekevu huku jasho ikimkimbia njia mbili mbili mashavuni.

“Huyu ni mgeni wetu?” Askari huyo aliyevalia sare zilizotawaliwa na maandishi “G4S” Alizidi kutuhoji. “Mimi niko tuu katika hali ya kujitafutia riziki hebu mhoji yeye si bubu” alijibu kama kwa dharau.

Nikivumilia harufu mbaya ya dereva huyo aliyenukia Kama beberu sikujua jinsi ningejinasua kutoka kwenye mtego huu. Mara tuu nilipo jaribu kushuka ndipo nilijipata nimeramba mchanga huku pikipiki ikipinduka na mizigo yangu kutapakaa ovyo ovyo.
Kando yangu alionekana dereva huyo naye akijipangusa mchanga kichwani, hapo ndipo nikabaini kwamba piki piki ile mbovu ilikuwa ni kama inalipiza kisasi kutokana na jinsi ilikuwa inadhulumiwa.

“Pole kwa ajali!” sauti nyororo ilinizindua kutoka ardhini. Kweli hakuna sababu ya kutofautiana na waliodai sauti nzuri humtoa nyoka pangoni. Hata baada ya mimi kubingiria na kujeruhi goti, nilijisikia ni kama sauti hiyo ilikuwa ni barafu ya kunipoza machungu.

Kabla hata ya kuvinjari maumbile ya mrembo huyu aliyekuwa amevalia minisketi iliyonakshiwa na umbo za duara ndipo nilisikia dereva wa pikipiki akifoka “wewe ni mshamba kutoka wapi, Unashuka kwenye pikipiki ni kama unashuka kutoka mgongoni mwa punda?”

Muungwana wanasema hanuni mashavuni ila hununa moyoni. hivyo, kwa upole nilinyanyuka na kumwachia fursa ya kuzidisha mashambulizi yake makali.

Nikielewa fika kwamba jogoo wa shamba daima hawiki mjini ilikuwa ni zamu yangu kuficha makucha na kunyenyekea huku waliotazama kisa hicho wakimlaaani dereva na kunionea imani “maskini mtoto wa watu!” alisikika mmoja akisema.

Kama kutonesha kidonda baradhuli huyo alizidi kuimarisha ukaidi wake “wee hebu nipe pesa zangu unafikiri nilikuwa nikifanya kazi ya kupaka mbwa rangi”
“Unamdai pesa ngapi?” mrembo huyo alidakia tena kwa ile sauti nyororo.

Bila ya kusita na kujiepusha na aibu zaidi niliingia mara moja mfukoni na kumchomolea noti ya shilingi hamsini. “Nimeshukuru kwa ukarimu wako lakini wacha tuu nibebe msalaba wangu mwenyewe” nilimjibu mrembo huyo.
* * *
Lucy Bahati alikuwa msichana mrefu, shingo ya chupa, kiuno cha nyigu na meno meupe yaliyo pangana kama chane kombani. Sisemi ngozi yake laini, nywele yake ya kipilipili na pia sitaji mavazi yake uliyojumlisha “tumbo cut” ya samawati, minisketi nyeusi yenye umbo za mraba na kumalizia na harufu hai ya waridi iliyomwandama kote. We! Hata wewe ungeathirika.

Tisheti yake ilitawaliwa na mandishi “look but don’t touch”. Utanisamehe kwani sikupata fursa ya kuomba kufafanuliwa maana yake.
“Ina makosa nikijua jina lako” nilimchokoza kwa ujanja.

“Ah! Mimi naitwa Lucy Bahati mmoja wa wanafunzi wakongwe chuoni humu. Kutokana na lahaja yake na ujuzi wa lugha mara moja nilibaini asili yake ni pwani.
“Na wewe waitwaje, naomba nikubebee hiyo godoro?” ilianzia hapo.

“Wananiita Rashid Mchristow ukipenda Mwana Maoni” nilimjibu bila ya kusita huku jibu langu likiibua kicheko kikubwa.

Comments

Nawakaribisha Nyote katika ukurasa huu kutoa maoni yenu pamoja na mafunzo kwani kando na Mwenyezi ambaye mpaka leo hajachoka kuongeza majira katika moyo wangu dhaifu ni myie ambao mmenipa maana ya maisha na sababu ya kuzidi kutumia kalamu yangu kuwafunza, kuwatumbuiza .......orodha hiwezi wkisha. kongole kwenu nyote!

Popular posts from this blog

MAZINGAOMBWE YA SAA

Na Danyell Odhiambo Nimejirusha kwenye kiti kilegevu cha msonobari nikifikiria jinsi hali ya maisha nchini Kenya inavyozidi kupaa kila uchao. Mbele yangu, pametulia redio, kando pamesimama kikombe cha kahawa chungu na juu pananinginia saa ya ukuta. Ghafla, fikra zangu zinatekwa nyara na saa iliyozubaa ukutani. Nikiangazaangaza, naona imetimia usiku mkuu. Hii ni kumaanisha, mishale yote ya saa imekutana kifuani pa namba kumi na mbili. Ukipiga hesabu kwa makini, utakubalina nami kwamba tukio kama hili hujirudia mara mia tatu sitini na tano kila mwaka. Ukumbuke, kisa hiki pia huashiria kuzaliwa kwa siku mpya. Hata ingawa mishale hizi zimedhibitisha ushirikiano ni kiungo muhimu katika katika kikundi, taswira fulani inaibuka nikiangalia mishale hizo. Taswira yenyewe yahusu tabia mbovu ya wabunge kukaidi shinikizo za kuwataka kulipa malimbikizi yao ya kodi. Nikipamabanua kitendawili hiki, itakubali kwamba jamii imejigawanya kupitia mishale hizi tatu za saa. Mahuluku taabu nawafa...

OPERATION TUTETEE WANAUME!!!

MTUNZI: ODHIAMBO DANYELL SEHEMU YA KWANZA: Mzee Matendechere alionekana kuokotwa na usingizi mwepesi wakati akiuguza majeraha ya panga hospitalini. Kisa na maana, adabu ilimhama mkewe hata akaamua kuchukua sheria mkononi na kumpa mumewe kichapo cha mbwa kabla ya kutorokea kusichojulikana. Kichwa chake kilibanwa kwa kilemba cheupe chenye matone ya dam u. Isitoshe, Kwenye shavu la kushoto, palidhihirika jeraha bichi lenye kushonwa kwa uzi. Cha kusikitisha zaidi, Pembezoni mwa kitanda, wangeonekana wapiga picha kutoka vyumba vya habari waking’ang’ana kuchukua picha za kuvutia watazamaji. picha kwa hisani ya http://medievalminds.com Maskini Matendechere alizidiwa na usingizi hata akabakia kukoroma huku akifungua mdomo mithili ya mamba mwenye njaa. “Wow! This seems to be the best shot, I,m loving this” alisikika akisema mmoja wa wapigaji picha tuliyeshuku ni wa asili ya kimarekani. Kweli, vita vya panzi furaha ya kunguru. Wakati haya yakijiri, ndoto ya m...

KUMBU KUMBU ZA MWANA HAWA

MTUNZI: Odhiambo Danyell Manyunyu mepesi ya mvua yangesikika yakikung’uta mabati na kuibua mdundo flani iliozidisha tamaa yangu ya  kuendelea kupanga mbavu kwenye kitanda. Mara, alisikika jogoo mmoja kijijini akiwika kama kuashiria nuru ilikuwa imekubali zamu yake ya mchana. Nilibaki kugaragara kitandani huku mabishano makali yakiendelea akilini kati ya mwili dhaifu na nafsi yangu. Mwili ilisisitiza niendelee kulala huku nafsi ikinisihi niamke. Baada ya kutafakari kuhusu hasara za usingizi niliridhia kuamka. Ghafla, fikra zangu zilielekezwa katika saa kubwa iliyoning'inia ukutani ambayo ilikatiza hali ya unyamafu uliokuwa umetawala chumbani. kuzidisha, chenene fulani aliyekuwa kajificha mvunguni alianza kutoa sauti ya kuudhi. “Aah! Heri tuu niamke” nilijisemeza huku nikijikokota kuelekea kwenye dirisha. Nikichungulia nje, ningeona kunguru wakipigania makombo ya chakula kwenye pipa iliyosimama mkabala na chumba changu. Isitoshe, rukwama kukuu za wazegaz...